Aya:
98
Mahali iliteremshwa:
Makka
Ali Muhsin Al-Barwani - Swahili Translation of Al-Muntakhab
SURAT MARYAM
(Imeteremka Makka)
Hii ni Sura iliyo teremka Makka, na hamna Aya za Madina ila Aya 57 na 71. Hisabu ya Aya zake ni 98. Imeanzia kwa harufi moja moja kama Sura nyingi nyenginezo. Ndani ya Sura hii kipo kisa cha kuzaliwa Yahya bin Zakariya (Alayhima Ssalam). Zakariya alitamani mwana na hali kesha fikilia ukongwe na mkewe ni tasa. Na kimetajwa pia kisa cha Bibi Bikra Maryam ((AS)) na kumzaa kwake Masihi ((AS)). Kisha kikatajwa kisa cha Ibrahim (A.S) na Wito wake kulingania Upweke Mwenyezi Mungu, na alivyo mtaka babaake aache kuabudu masanamu, na majibizano wa yao yaliyo jiri kwa ajili ya masanamu, na madaraka ya Shetani.
Pia wameashiriwa Manabii wengine katika dhuriya za Ibrahim, nao ni Ismail na Is-haq na dhuriya wa Is-haq. Tena kikagusiwa kisa cha Idris ((AS)). Na tena Mwenyezi Mungu Subhanahu akataja khabari za walio fuatia wakaja baada ya Manabii, watu watiifu na wengine maasi. Na akataja kuwa Pepo ndiyo malipo ya Waumini, na Moto ni malipo ya makafiri, na akazitaja hali za makafiri katika Jahannamu. Na tena Subhanahu akagusia ya wapotovu wanao sema kwamba Mwenyezi Mungu ana mwana.
Na Subhanahu amebainisha cheo cha Qur'ani, na amewaonya makafiri, na amepiga mifano ya watakavyo teketea wanao waasi Manabii. Na akaashiria kwamba hao wamepotea kabisa, hawakuacha hata ukumbusho.